Friday, December 21, 2007

Jumamosi Desemba 22,2007.

SHINIKIZO LA JUU LA DAMU (HYPERTENSION)

Wapendwa wasomaji katika makala ya leo ambayo ndiyo ya kwanza katika blogu hii tutatazama Ugonjwa wa shinikizo la juu la damu ambao kwa lugha ya Kitaalamu huitwa “Hypertension” au kwa lugha ya Kigeni “High Blood Pressure”. Ugonjwa huu ni moja ya magonjwa yanayowaathiri watu duniani kutokana na mateso,vifo pamoja na gharama zinazoambatana nao.Ugonjwa huu umekuwa ni moja ya changamoto muhimu katika afya ya jamii
Utangulizi
Kwa kawaida wakati moyo ukisukuma damu katika ateri (mishipa midogo ya damu),damu hiyo hupita kwa nguvu dhidi ya kuta za mishipa hiyo.
Shinikizo la damu hupimwa na kifaa maalum kijulikanacho kitaalum kama sfigmomanometa (sphygmomanometer) na kuweka damu kwa tarakimu mbili kwa mfano 120/80 milimita za mekyuri (zebaki)
Namba ya juu huonyesha shinikizo litakanalo na kutanuka na kusinyaa kwa moyo wakati damu ikisukumwa kutoka katika chemba za moyo kitaalamu huitwa systolic pressure. Namba ya chini yenyewe huonyesha shinikizo katika mishipa ya damu (ateri) wakati damu ikijaa kwenye chemba za moyo kwa kitaalumu huitwa diastolic pressure.
Kipimo cha kawaida cha shinikizo la damu kwa watu wengi ni milimita za mekyuri 120/80 .Chini ya hapo huitwa shinikizo la chini la damu (hypotension) na juu ya kipimo hicho huitwa shinikizo la juu la damu (hypertension) ambalo huanzia milimita za mekyuri 140 kwa “systolic pressure” milimita za mekyuri 90 kwa “diastolic pressure”.
Shinikizo la juu la damu lisilotibiwa linahusishwa na vifo vingi na madhara ya tokanayo na kusimama kwa moyo, kiharusi na figo kushindwa kufanya kazi. Kutokana na tafifi mbalimbali zilizofanywa, hatari ya kufa kutokana na moyo kusimama na inahusishwa moja kwa moja na shinikizo la damu haswa kipimo cha “sistoliki” (systolic). Hata hivyo ongezeko la magonjwa ya moyo kutokana na shinikizo la juu la damu linaweza kupunguzwa.
Nini husababisha shinikizo la damu?
Kuna aina mbili za shinikizo la juu la damu ;
Shinikizo la juu la damu la lazima (Essential Hypertension)

Aina hii ya shinikizo la juu la damu huathiri kati ya asilimia 90-95% ya watu wanaougua shinikizo la juu la damu.Hata hivyo hakuna sababu ya kisayansi ya uhakika iliyokwisha kutolewa kuelezea kwa nini ingawa kuna baadhi ya vigezo vinaorodheshwa kuhusika na shinikizo hilo la juu la damu.
Vigezo visivyobadilika:
Umri:Kadri umri unavyoongezeka ndivyo uwezekano wa kupata shinikizo la juu la damu unavyozidi kuwa mkubwa kwa sababu kuta za mishipa ya damu huzidi kuwa ngumu hivyo kushindwa kutanuka kirahisi na kuongeza shinikizo (pressure)
Asili (Race): Jamii ya watu weusi (waafrika) wana hatari kubwa zaidi kupata shinikizo la damu kuliko watu weupe.
Histori a ya Kifamilia (Kurithi): Imegundulika kuwa uwezekano wa ndugu kupata shinikizo la juu la damu ni mkubwa iwapo ndugu wengine katika familia wamekwishawahi/wanaugua ugonjwa huo.
Jinsia:Wanaume wana uwezekano mkubwa zaidi wa kupata shinikizo la juu la damu kuliko wanawake.
Vigezo vinaivyobadilika:
Hivi ni vile ambavyo kwa lugha nyingine vyaweza kuepukwa.
Unene wa kupita kiasi: Unene wa kupita kiasi ni uzito wa zaidi ya “body mass index” (BMI) 30kg/m2 (BMI =uzito (kwenye kg) ÷ Urefu (kwenye mita)2 )

Kiwango cha chumvi (sodium) mwilini : Baadhi ya miili ya watu hugundua haraka kiwango cha chumvi (sodium) na shinikizo lao la damu hupanda punde watumiapo chumvi.Kupunguza matumizi ya chumvi husaidia kupunguza shinikizo la damu. Vyakula vya viwandani na madawa ya kupunguza maumivu huwa na kiasi kikubwa cha madini ya chumvi “sodium”
Vidonge vya majira: Baadhi ya wanawake wanaotumia vidonge vya uzazi wa majira hupata shinikizo la juu la damu.
Kutokufanya mazoezi: Kutokufanya mazoezi ni moja ya sababu zinazopelekea unene wa kupita kiasi (obesity).
Madawa: Baadhi ya madawa kama Amphetamines huweza kupandisha shinikizo la damu.

Shinikizo la juu la damu litokanalo na magonjwa mengine (Secondary hypertension)
Aina hii ya shinikizo huathiri karibu asilimia 10 ya watu.Hutokana na magonjwa mengone kama:
-Magonjwa sugu ya figo
-Uvimbe kwenye tezi za figo (adrenal gland)
-Kupungua kwa upana wa mshipa mkuu tuoao damu kwenye moyo kwena mwilini (coarctation of aorta)
-Ujauzito
-Matumizi ya vidonge vya majira
-Matumizi ya kupita kiasi ya pombe
-Kutokufanya kazi kwa tezi mdundumio (thyroid gland dysfunction)
-Madawa na sumu (kokeini)
Dalili za Shinikizo la Juu la Damu
Kwa kawaida Shinikizo la juu la damu huwa halionyeshi dalili na kama zikitokea basi huwa kwa kiasi kidogo na zisizo maalum na ndio maana ugonjwa huu huitwa “Muuaji wa Kimya kimya” (Silent Killer).Watu wenye Shinikizo la juu la damu huwa hawajifahamu mpaka wanapopimwa.
Baadhi ya watu wenye shinikizo la juu la damu huwa na dalili zifuatazo:
-Maumivu ya Kichwa
-Kizunguzungu
-Kutoona sawasawa
-Kichefuchefu
-Kichomi
-Kuchoka haraka
Uchunguzi na Vipimo
Kupima Shinikizo la damu kwa kutumia Mashine ya Kupimia Presha ili kujua kama ni zaidi ya Milimita za Mekyuri 140/90.
Damu: Kuangalia kiwango cha Yurea (urea),madini (electrolytes) na Krietinini (Creatinine)
Kiwango cha Mafuta (Lipid profile) kuangalia aina tofauti za lehemu (cholesterol)
Vipimo maalum vya homoni za tezi za figo (adrenalini) and tezi mdundumio (thyroid)
Mkojo kutazama madini (electrolytes) au homoni
Mionzi ya sauti (ultrasound) kutazama kama figo zimeharibika au kuvimba
Echocardiagram (ECHO) kuchunguza kama moyo umetanuka mabadiliko yoyote yasiyo ya kawaida kwenye mishipa ya moyo au valvu.

Viungo au mifumo iathirikayo na shinikizo la juu la damu
Mfumo was fahamu (Central Nervous System): Kuvuja kwa damu kwenye ubungo (interecerebral hemorrhage), kiharusi (stroke)

Mfumo wa kuona /macho (ophthalmologic): Kuvunja damu kutokana na kupasuka kwa mishipa midogo ya damu (fundal hemorrhages)

Moyo: Kutanuka kwa ventriko ya kushoto ya moyo (left ventricular hypetrophy) ambayo kupungua kwa kiwango cha damu kisukumwacho na moyo maumivu ya moyo (Angina Pectoris).
Mishipa ya damu: kuharibika kwa mishipa (diffuse atherosclerosis)
Figo: kudhurika kwa mishipa ya damu kwenye figo (Nephrosclerosis), kuziba kwa mishipa ya damu ipelekayo damu kwenye figo (renal artery stenosis)

Kinga
Jali uzito wako kwa kutonenepa kupita kiasi
Kufanya mazoezi pia hupunguza uzito
Punguza kiwango cha chumvi kwenye chakula
Punguza kiwango cha pombe ( si zaidi ya bia tatu (3) kwa Mwanaume na bia (2) kwa siku kwa mwanamke
Kula mlo wenye matunda na mboga za majani zaidi, samaki, maziwa, samli nk
Punguza vyakula vyenye mafuta haswa lehemu (cholesterol)
Acha kuvuta tumbaku (sigara)
Punguza msongo wa mawazo (stress) kwa kufanya mazoezi, yoga n.k

Matibabu na Ushauri
Shinikizo la juu la damu ni ugonjwa wa muda mrefu (kudumu) na ili udhibitiwe, mabadiliko katika mwenendo wa kuishi (litestyle) na matumizi sahihi na endelevu ya dawa lazima yazingatiwe.Ni muhimu kujenga utamaduni wa kupima shinikizo la damu mara kwa mara kwa sababu mara nyingine dalili huchelewa kuanza kuonekana.
Upasuaji
Upasuaji waweza kuhitajika kama kuna uvimbe katika tezi za figo (adrenal glands) ambazo zinatengeneza homoni.
Kuziba kwa mshipa upelekao damu kwenye figo (narrowing of renal artery) kunaweza kufanya upasuaji kufanyika kurekebisha tatizo.
Onana na daktari wako kama una dalili zilizotajwa hapo juu,usitumie dawa yoyote bila ushauri wa daktari.
Dondoo za kubadili tabia
1. Tumia ngazi badala ya lifti
2. Paki gari mbali kidogo kutoka kwenye ofisi
3. Endesha baiskeli
4. Jishughlishe na bustani
5. Fanya usafi wa nyumba
6. Cheza muziki
______________________________________________________
©http://ringomoses.blogspot.com 2007
*Si ruhusa kuinakili,kupunguza au kuongeza kitu katika makala hii au kuitumia bila ruhusa toka kwa Mwandishi wa Makala hii.Dkt. Ringo Moses, Simu:+255-713-550032 Barua pepe: ringomoses@yahoo.com au ringomoses@gmail.com*
______________________________________________________
(Makala hii inapatikana pia katika Gazeti la Majira Jumapili la Tarehe 28 Oktoba 2007)