Tuesday, January 8, 2008

JINSI YA KUISHI NA MTU MWENYE UGONJWA WA KIFAFA

Karibuni tena wapenzi wasomaji katika makala hii ya Daktari wako.Jumapili ya leo tutaangalia jinsi ya kuishi na mtu mwenye kifafa kwa kutazama dalili za awali,vigezo hatarishi,uchunguzi uambatanao na ugonjwa wa kifafa na hatua za kuchukua iwapo mtu amepatwa na kifafa.

Utangulizi
Ubongo wa binadamu umeundwa na zaidi ya seli za neva (seli za fahamu) bilioni mia moja.Seli hizi zote huwasiliana ambapo baadhi huzichokoza nyingine kutuma jumbe zaidi wakati nyingine huzifanya nyingine kutotuma ujumbe kama inavyotakiwa.Utendaji mzuri wa ubongo unategemea uwiano katika kutuma ujumbe.Utumaji usio na udhibiti hupelekea mlipuko wa umeme katika seli za ubongo ambapo huweza kupelekea mtu kupata kifafa (seizure) hali ambayo huambatana na kupoteza fahamu,kuzubaa,kukakamaa misuli,kuchanganyikiwa au kuchezesha viungo haswa mikono na miguu.
Sote tuko katika hatari ya kupata kifafa.Kifafa chaweza tokea bila sababu dhahiri lakini watu waliowahi kudhurika ubongo wako katika nafasi kubwa ya kupata kifafa. Kifafa hakirithiwi ingawa mara chache hutokea hivyo na zaidi haswa kwa ndugu ambao wana muathirika wa kifafa.

Aina za Kifafa
Kuna aina kuu mbili za kifafa,nazo ni Kifafa Kamili (Generalised seizure) na Kifafa Upande (Partial seizure).
Kifafa Kamili (Generalised seizure)
Kifafa cha aina hii huwa na milipuko ya umeme katika seli za fahamu za ubongo mzima au sehemu kubwa ya ubongo.Aina hii ya kifafa huambatana na kupoteza fahamu.
Kifafa Upande (Partial seizure)
Katika aina hii ya Kifafa sehemu tu ya ubongo huwa imeathirika.Dalili hutegemea sehemu husika ya ubongo iliyodhurika.Si kawaida kwa waathirika wa aina hii ya kifafa kupoteza fahamu.Waathirika wake hupatwa na mishtuko ya misuli haswa mikono na miguu.
Vigezo hatarishi vya mtu kupata kifafa
Vifuatavyo ni baadhi tu ya vigezo hatarishi ambavyo vyaweza kupelekea mtu kuathirika na ugonjwa wa kifafa:
-Watoto waliozaliwa njiti
-Watoto wapatao kifafa katika mwezi wa kwanza mara tu baada ya kuzaliwa
-Kuvujia damu kwenye ubongo
-Kuwa na mishipa yenye matatizo kwenye ubongo
-Madhara makubwa kwenye ubungo
-Ukosefu wa hewa ya oksijeni ya kutosha kwenye ubongo
-Saratani ya ubongo
-Magonjwa yanayoathiri ubungo kwa mfano homa ya uti wa mgongo
-Kiharusi
-Historia ya kuwepo kwa kifafa au degedege liambatanalo na homa katika familia
-Utumiaji wa dawa za kulevya kama kokeini
-Madhara ya wastani kichwani na kupoteza fahamu kwa muda

Sababu zipelekeazo mtu kupata kifafa
Kwa zaidi ya theluthi mbili ya wagonjwa wa kifafa hakuna sababu maalum iliyogundulika ila kitendo cha historia ya uwepo wa kifafa kwenye familia inaashiria kuwepo kwa sababu za kijenetiki.
Sababu zifuatazo pia zinahusishwa:
-Madhara kwenye kichwa
-Operesheni ya kichwa
-Magonjwa ya ubongo kama homa ya uti wa mgongo
-Kiharusi
-Saratani ya ubongo
-Unywaji pombe wa kupindukia
-Kupungua chini ya kiwango kwa sukari katika damu (hypoglycemia)
Pia mpendwa msomaji ni vyema ukafahamu vitu ambavyo vinaweza kuchokoza kifafa.Hivi si vingine bali ni:
-Mwanga mkali kama wa flashi ya kamera, taa ya gari, runinga n.k
-Homa kali
-Msongo wa mawazo na kutolala
-Kilevi
-Dawa za kulevya kama kokeini, heroini n.k
-Homoni.Wakati estrojeni zinapokuwa juu au projestroni kushuka.Hii yaweza kutokea siku chache kabla ya kuingia kwenye hedhi au wakati wa hedhi au wakati wa kutolewa kwa yai (ovulation).
-Madawa haswa yale ya magonjwa ya akili
-Upungufu wa virutubisho (nutritional deficiencies)
Dalili za mwanzo za tahadhari za kifafa
-Kutoona vizuri
-Kujisikia vibaya/ kiajabuajabu
-Kuogopa
-Kizunguzungu
-Kichefuchefu
-Kusikia kama vitu vikikutambaa mwilini
-Kusikia ganzi
Hata hivyo kifafa chaweza kuja bila dalili za wawli za tahadhari.Dalili zifuatazo zaweza tokea:
-Kupoteza fahamu kwa ghafla (black out)
-Kuchanganyikiwa
-Kuzimia
-Kupoteza uwezo wa kuona
-Woga
-Kutafuna tafuna ulimi
-Kupata shida ya kuongea
-Kutoa mate
-Kuviringisha macho
-Kudondoka
-Kutupa tupa miguu
-Kupunga mkono
-Kushindwa kujizuia haja (kubwa/na ndogo)
-Kushindwa kusogea
-Kujilamba midomo
-Kuduwaa
-Kukakamaa
-Kutoa jasho
-Kutetemeka
-Kupumua kwa shida
-Kubana /kusaga meno
-Moyo kwenda mbio
Baada ya kifafa wagonjwa wa kifafa huwa na dalili zifuatazo:
-Kupoteza kumbukumbu
-Kuchanganyikiwa
-Kuwa na mfadhaiko (majonzi)
-Maumivu ya kichwa
-Kichefuchefu
-Michubuko
-Maumivu
-Kiu
-Kuchoka
-Hamu ya kujisaidia (haja kubwa au ndogo)
Nini cha kufanya iwapo mgonjwa wa kifafa amepatwa na kifafa
-Ondosha vitu vyovyote vinavyoweza kumdhuru kama moto n.k
-Usijaribu kumzuia kurusha miguu au mikono
-Usimuhamishe kumpeleka mahala pengine
-Mgeuze upande (kiubavu) ili kama kuna kimiminika chochote mdomoni kiweze kutoka
-Toa nguo yoyote iliyobana shingoni ili aweze kupumua vizuri
-Kaa naye mpaka apate fahamu (yaweza kuchukua mpaka dakika kumi na tano)
Usifanye yafuatayo:
-Kuweka kitu chochote mdomoni
-Kujaribu kumzuia mgonjwa asirushe mikono au miguu

Uchunguzi
Vipimo vifuatavyo ni muhimu kutokana na uwezo wa mgonjwa katika kugundua chanzo cha tatizo kwenye ubongo kiletacho kifafa:
Kipimo cha Kompyuta cha Kuchunguza ubongo (CT Scan);Kipimo hiki huonyesha sehemu mbalilmbali za ubongo kuchunguza kama kuna athari yoyote.
Kipimo kingine ni cha electroencephalogram (EEG) ambacho husaidia kufuatilia hali ya utendaji wa kiumeme wa seli za ubongo.
Kipimo kingine cha uhakika zaidi lakina aghali ni cha kuchunguza ubongo kwa usumaku Magnetic Resonance Imaging (MRI).
Matibabu na Ushauri
Ni vyema kumuona daktari aliye karibu nawe iwapo una tatizo au una mtu mwenye tatizo la kifafa.Kumbuka mtu mwenye kifafa anaweza kuishi maisha ya kawaida kama mtu mwingine iwapo atadhibiti dalili na kunywa dawa kama alivyoelekezwa na daktari.Hakikisha unafuata maelekezo ya daktari wako kuhusu matumizi ya dawa na epuka kuacha kunywa pombe wakati ukiendelea na matibabu.Endelea na matibabu hata pasipo na dalili, wasiliana na daktari wako kabla ya kuacha kutumia dawa.Pia ifahamike kwamba kifafa si ugonjwa wa akili na si ishara ya kuwa na uwezo mdogo kiakili.
____________________________________________________
©http://ringomoses.blogspot.com 2007
Si ruhusa kuinakili, kupunguza au kuongeza kitu katika makala hii au kuitumia bila ruhusa toka kwa Mwandishi wa Makala hii. Dkt. Ringo Moses, Simu: +255-713-550032 Barua pepe: ringomoses@yahoo.com, ringomoses@gmail.com
(Makala hii inapatikana pia katika Gazeti la Majira Jumapili la Tarehe 4 Novemba 2007)
______________________________________________

No comments: